MWANANCHI
Polisi Kilimanjaro inamshikilia mzee
Mungai Molel (75) kwa tuhuma za kumbaka mtoto wa miaka 11 wa shule ya
msingi Okaseni na kumjeruhi vibaya katika sehemu za siri.
Kamanda wa Polisi mkoani humo Geofrey
Kamwela amethibitisha kutokea kwa tukio hilo liliotokea Novemba 12,
Kijiji cha Kitandu kata ya Uru Kusini ambapo mtuhumiwa huyo alimwita
mtoto huyo nyumbani kwake na kumfanyia kitendo hicho cha kikatili.
“Alimwita nyumbani kwake na kumbaka na
kumsababishia maumivu makali sehemu za siri na kusababisha mtoto huyo
kulazwa katika Hospitali ya KCMC kwa matibabu kutokana na kuharibika
vibaya sehemu za siri” — Kamwela.
Alisema mzee huyo alimbaka mtoto huyo
hali iliyosababisha mtoto huyo kupiga kelele na kuokolewa na majirani wa
mzee huyo na kutoa taarifa Polisi baada ya kumkuta mtoto huyo akivuja
damu nyingi.
Mtuhumiwa huyo anashikiliwa na Jeshi la Polisi kwa uchunguzi zaidi na atafikishwa mahakamani upelelezi utakapokamilika.
MWANANCHI
Hakimu wa Mahakama ya Mwanzo ya Mengwe
Adinani Kingazi, amemhukumu kifungo cha miaka mitatu jela Godfrey
Kimaria (35) baada ya kukutwa na hatia ya kumjeruhi mtoto wa miaka minne
kwa kumg’ata mgongoni akimtuhumu kumuibia paka.
Kesi hiyo ilivuta hisia za watu Wilayani
Rombo Mkoani Kilimanjaro ambapo wananchi walifurika katika mahakama
hiyo kusikiliza hukumu ya kesi hiyo.
Akitoa hukumu hiyo hakimu Kingazi
alisema tarehe 29 Septemba mwaka huu katika Kijiji cha Msera juu,
mshtakiwa alifanya kosa hilo kinyume cha kifungu cha sheria 214 cha
sheria ya makosa ya jinai.
Hakimu huyo alisema mshtakiwa alifanya
ukatili huo kwa mtoto Dilex Lyakurwa (09), ambapo mshtakiwa
alimshambulia mtoto huyo kwa kile alichodai kuwa mtoto alienda kuchota
maji nyumbani kwake, wakati akiwa anarudi kwenda nyumbani paka wa
mshtakiwa alimfuata mtoto, baadaye paka huyo aligoma kurudi, ndipo
mshtakiwa alimshambulia kwa madai kuwa amemuibia paka wake.
Mahakama imeridhishwa na ushahidi
uliotolewa na upande wa mashtaka pamoja na vielelezo vya Polisi ikiwemo
taarifa ya Daktari iliyoonyesha mtoto huyo aliumizwa kwa kuchomwa na
kitu chenya ncha kali mgongoni.
Mshtakiwa anatumikia kifungo cha miaka
mitatu jela na baada ya kumaliza adhabu atamlipa mlalamikaji shilingi
laki mbili kama gharama za matibabu na fidia ya maumivu aliyoyapata.
NIPASHE
Mkuu wa Wilaya ya Korogwe Mrisho Gambo, ameliagiza Jeshi la Polisi na
Mkurugenzi wa halmashauri ya Wilaya ya Korogwe Lucas Mweri, kumchukulia
hatua daktari anayedaiwa kumbusu mgonjwa wake wakati akimpa matibabu.
Gambo alitoa agizo hilo baada ya kupokea malalamiko ya tukio hilo na
kueleza kuwa ni ukiukwaji wa maadili ya Udaktari na aibu kwa Wilaya.
Aliliagiza Jeshi la Polisi kufanya uchunguzi na kuchukua hatua za
kisheria ili iwe fundisho kwa mtaalam huyo na wengine wenye tabia kama
hiyo.
Inadaiwa daktari Ally Naah anayefanya kazi Hospitali ya Wilaya ya
Magunga, anadaiwa kumbusu mwanamke aliyekuwa akimpatia matibabu
Hospitalini hapo.
Mashuhuda wanasema siku ya tukio mwanamke huyo aliongozana na mume
wake kwa ajili ya kupata matibabu na baada ya kufika Daktari alimtaka
aingie ndani kumfanyia uchunguzi, huku mume wake akiwa nje akimsubiria
na baada ya kumsubiria kwa muda mrefu alipata hofu, ndipo alipochungulia
dirishani na kumkuta daktari akimbusu mke wake.
“Yule bwana hakuamini alichokiona hakuvumilia alipiga kelele kuomba
msaada.. kwa kweli jambo hili ni aibu na limetuondolea uaminifu” alisema
mmoja wa shuhuda wa tukio hilo ambalo tayari Polisi wameanza kulifanyia
uchunguzi.
Mganga mkuu wa wilaya ya Korogwe, Dk Olden Ngasa amethibitisha
kutokea kwa tukio hilo na kusema daktari huyo alitoroka baada ya tukio
hilo.
HABARI LEO
Watoto watatu kutoka kijiji cha Barca
huko Arber Wilayani Oyam Uganda, wanazungumza lugha isiyofahamika baada
ya kufungiwa ndani ya nyumba yao kwa miaka saba, Lugha hiyo mpya
imetajwa na watu wa jamii hiyo kuwa Leb-ad-am, ikimaanisha lugha ya
ubongo.
Inadaiwa Baba wa Watoto hao aliwafungia
ndani ili kuwalinda kutokana na hatari mbalimbali, watoto hao
hawajaathirika kiakili bali hawawezi kuzungumza na watu wengine huku
wakiamini kile baba yao anachowaambia.
Mama yao amesema watoto hao waliweza
kuishi kwa kula mayai ya Chura yaliyochemshwa na majani, ambayo hula
kila asubuhi na jioni na kutumia maji kutoka katika shimo lililochimbwa
na baba yao.
Baba wa watoto hao alimzuia mama yao
kuzungumza nao kwa kipindi chote, hatua hiyo iliwafanya kutojifunza
lugha yao ya Kiluo wakati walipokuwa wadogo.
MTANZANIA
Jeshi la Polisi Mwanza limemfukuza kazi Askari wake Sajini WP Fatuma,
baada ya kudhibitika kuwa alimkata vidole vinne mfanyakazi wake wa
ndani Steven Magesa(18)
Kamanda wa Polisi Mwanza Valentine Mlowola, alisema baada ya kupokea
taarifa za tukio la Askari huyo lililotokea Oktoba 20 mwaka huu ,
walichukua hatua za kiutawala na kuanza kufanya uchunguzi kufuatia tukio
hilo, lililofanyika katika Kijiji cha Magange Mugumu Wilayani Sengerema
Mkoani Mara ambapo ni nyumbani kwa kijana huyo, na walipata udhibitisho
wa kutosha wa Askari huyo kuhusika na kosa hilo, hivyo kumfukuza kazi
baada ya kumsikiliza katika Mahakama ya Jeshi.
“Baada ya uchunguzi tulibaini kuwapo kwa udanganyifu wa maelezo
yaliyotolewa na WP Fatuma kuhusiana na tulkio hilo, hivyo kutokana na
ushahidi uliowasilishwa katika Mahakama ya Jeshi, tulimtia hatiani na
kuvuliwa nyadhifa zake zote ikiwa ni pamoja na kumfukuza kazi,
“Kwa sasa WP Fatuma amesafirishwa kwenda Mkoani Mara kwa ajili ya
kushitakiwa Mahakamani kwa kosa la Jinai, hili ni fundisho kwa Askari
wetu wengine wenye tabia kama hii na watu wengine ambao wamekuwa
wakijichukulia sheria mkononi na kufanya vitendo vya Jinai kwa kushindwa
kufuata sheria”, alisema Mlowola.